Maandamano Tanzania: Miji mikuu yabaki tulivu asubuhi ya Disemba 9 huku tahadhari zikiongezeka
Huku leo Disemba 9, siku ambayo pia ni kumbukumbu ya Uhuru wa Tanzania bara, ikiwa ndio siku iliyotajwa kwa maandamano yaliyopigwa marufuku, hali katika maeneo kadhaa ya nchi hiyo imeripotiwa kuwa tulivu asubuhi hii lakini yenye tahadhari kubwa.
Ingawa hakuna mikusanyiko iliyoonekana mapema leo, shughuli nyingi za biashara zimeendelea kubaki zimefungwa kama njia ya kujilinda endapo machafuko yatatokea.
Waandishi wa BBC wameshuhudia baadhi ya vituo vya mafuta, maduka na ofisi binafsi pamoja na za umma zikiwa zimefungwa, hatua inayohusishwa moja kwa moja na kumbukumbu ya maandamano ya Oktoba 29 ambayo yalisababisha uharibifu mkubwa wa mali.
Kwa mujibu wa takwimu za awali zilizotolewa na serikali, maandamano hayo yaliharibu ofisi za serikali zipatazo 756, vikaharibu vituo 27 vya mabasi ya mwendo kasi pamoja na mabasi 6 yaliyoteketezwa. Nyumba binafsi 273 zilipigwa au kuchomwa, vituo vya polisi 159 vilishambuliwa, na vituo binafsi vya mafuta 672 navyo viliharibiwa. Aidha, magari binafsi 1,642, pikipiki 2,268, na magari ya serikali 976 yaliteketezwa katika machafuko hayo, hali iliyowaacha wananchi wengi na kumbukumbu nzito kuhusu athari za vurugu hizo.




No comments