Katika siku ambayo baadhi ya watanzania walitarajia kushuhudia hatua ya kihistoria ya maandamano ya amani ya Desemba 9, hali ilikuwa tofauti kwa siku nzima.

Hakukuwa na misafara ya waandamanaji, mabango, wala makundi makubwa ya watu kupaza sauti zao. Ilikuwa tofauti na maandamano ya Oktoba 29, 2025 na siku zilizofuata.

Badala yake, kulikuwa na utulivu wa tahadhari katika miji mikubwa iliyokumbwa na maandamano ya awali, utulivu ambao si wa ukimya, bali ulizungukwa na maswali mengi.

Si Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Mbeya, Kilimanjaro, Iringa au Dodoma kulikuwa na maandamano kama yale ya siku tatu kuanzia Oktoba 29, 2025 siku ya uchaguzi Mkuu.